Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa hali ya hewa wa siku 10 kuanzia leo, Jumapili, Juni 1, 2025, ikionya juu ya mvua na radi zinazotarajiwa kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Kwa mujibu wa utabiri huo, maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria yakiwemo mikoa ya Kagera, Geita, Shinyanga, Mwanza, Simiyu na Mara yanapaswa kujiandaa na hali ya mvua.
“Tutarajia mvua zilizoambatana na radi katika baadhi ya maeneo, hasa katika Kanda ya Ziwa,” TMA ilisema kupitia taarifa rasmi iliyotolewa kwenye tovuti yake.
Nyanda za juu kaskazini mashariki, zinazojumuisha mikoa ya Arusha, Manyara, na Kilimanjaro, pia zinatarajiwa kupata mvua nyepesi katika maeneo machache.
Wakati huohuo, pwani ya kaskazini inayojumuisha Tanga, kaskazini mwa Morogoro, Mkoa wa Pwani, Dar es Salaam, pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba — inatarajiwa kuandamwa na upepo mkali na mvua za hapa na pale.
“Katika maeneo haya ya pwani, tunatarajia vipindi vya upepo mkali na mvua za hapa na pale,” taarifa ilieleza.
Mikoa ya magharibi kama Kigoma, Katavi na Tabora itapata mvua za mara kwa mara na radi katika maeneo machache. Kinyume chake, hali ya ukavu inatarajiwa kuendelea katika mikoa ya kati kama Dodoma na Singida.
Nyanda za juu za kusini magharibi ambazo ni Rukwa, Songwe, Mbeya, Njombe, na Iringa pia zinatarajiwa kubaki kavu kwa kiasi kikubwa.
“Sehemu kubwa ya ukanda wa kusini, ikiwa ni pamoja na Ruvuma na maeneo ya kusini mwa Morogoro, inatarajiwa kuendelea kuwa na hali ya ukavu,” mamlaka hiyo ilisema.
Kwa upande wa pwani ya kusini inayojumuisha Mtwara na Lindi, TMA imetabiri vipindi vya upepo mkali na mvua katika baadhi ya maeneo.
Comments
Post a Comment