Mashabiki wa soka waanzisha ghasia baada ya ushindi wa PSG.

Klabu ya soka ya Paris Saint-Germain imeshinda Ligi ya Mabingwa kwa mara ya kwanza.

Mashabiki walizua ghasia baada ya Paris Saint-Germain (PSG) kutwaa taji lao la kwanza kabisa la UEFA Champions League, wakiifunga Inter Milan kwa kipigo cha kihistoria cha 5-0 katika fainali iliyofanyika mjini Munich.

Timu hiyo kubwa ya Ufaransa iliandika historia kwa kuwa klabu ya kwanza kushinda fainali ya Ligi ya Mabingwa kwa tofauti ya magoli matano, ikithibitisha ubabe wao kwenye jukwaa kubwa zaidi barani Ulaya. Mchezaji wa PSG, Désiré Doué, alikua mchezaji wa sita katika historia ya UEFA Champions League kufunga bao na kutoa pasi ya bao katika fainali.

Huko Paris, shangwe kubwa zililipuka huku mashabiki wakijaa mitaani, wakipeperusha skafu za PSG kutoka madirishani mwa magari na kufyatua fataki kusherehekea ushindi huo wa kihistoria. Hata hivyo, sherehe hizo ziligeuka kuwa vurugu katika eneo la Champs-Elysées, ambako polisi walilazimika kutumia mabomu ya machozi na pilipili kuwatuliza waandamanaji.

Msemaji wa polisi alisema kuwa gari moja liliwashwa moto karibu na Parc des Princes na akaongeza kuwa watu kadhaa walikamatwa kufikia mwisho wa usiku.

Huko Munich, picha za video zilionesha mashabiki wa PSG na Inter wakipigana vikali katika usafiri wa umma, chupa zikirushwa na makonde kurushwa. Kwa mujibu wa vyombo vya habari, angalau shabiki mmoja wa PSG alijeruhiwa katika shambulio la kushtukiza kwenye kituo cha treni cha chini ya ardhi cha Universitat, huku ripoti zikidai kwamba wahuni wa Inter walikuwa na silaha za makali.

Ghasia hizo zinaonyesha uhasama mkali unaojitokeza mara kwa mara wakati wa mechi za Ulaya zenye ushindani wa juu.







Comments