Pentagon kubadilisha jina la meli ya kivita ya Marekani yenye jina la 'shoga' – vyombo vya habari

Waziri wa Ulinzi Pete Hegseth ameripotiwa kuagiza meli ya Marekani USNS Harvey Milk kubadilishwa jina.

Jeshi la Wanamaji la Marekani limeelekezwa kubadilisha jina la meli ya USNS Harvey Milk, meli ya mafuta ya kijeshi iliyopewa jina la mwanaharakati wa haki za mashoga aliyeuawa na pia mkongwe wa Jeshi la Wanamaji, kama sehemu ya juhudi pana za Rais Donald Trump za kuondoa marejeo ya utofauti, usawa, na ujumuishaji (DEI) ndani ya jeshi.

Kubadilishwa kwa jina hilo bado hakujathibitishwa rasmi, lakini kumeelezwa katika waraka wa ndani, kwa mujibu wa vyanzo kadhaa vya ulinzi vilivyozungumza na Military.com na vyombo vingine vya habari vya Marekani siku ya Jumanne.

Meli ya USNS Harvey Milk ilipewa jina hilo mwaka 2016 na aliyekuwa Waziri wa Jeshi la Wanamaji wakati huo, Ray Mabus, kwa heshima ya huduma na harakati za Milk, na ilizinduliwa rasmi mwaka 2021 na mkongwe aliyebadili jinsia.

Milk, ambaye alikua ikoni ya jamii ya LGBT nchini Marekani kama afisa wa kwanza aliyejitangaza kuwa shoga aliyechaguliwa katika jimbo la California, aliwahi kutumikia Jeshi la Wanamaji la Marekani katika miaka ya 1950 kabla ya kufukuzwa kutokana na mwelekeo wake wa kingono. Mwaka 1978, chini ya mwaka mmoja baada ya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa bodi ya wasimamizi wa jiji la San Francisco, Milk aliuwawa kwa kupigwa risasi na mwanachama mwenzake wa bodi hiyo aliyekuwa na migongano naye kuhusu sera za jiji.

Kubadilishwa kwa jina hilo kunaendana na juhudi za utawala wa Trump za kurejesha “utamaduni wa wapiganaji” na kuondoa mipango ya utofauti, usawa na ujumuishaji (DEI) katika mashirika ya serikali ya shirikisho.

Maafisa waliotoa taarifa hizo kwa masharti ya kutotajwa majina yao, ili kujadili maamuzi ya ndani, walisema kuwa jina jipya la meli hiyo bado halijachaguliwa.

Uamuzi huo, unaokuja wakati wa Mwezi wa Fahari (Pride Month), umekosolewa vikali na Wademokrasia, ambapo Spika wa zamani wa Bunge la Wawakilishi, Nancy Pelosi, alilaani hatua hiyo kama “kitendo cha aibu na cha kulipiza kisasi cha kufuta historia ya watu waliopigania haki za raia.”

Gavana wa California, Gavin Newsom, naye alikemea uamuzi huo na kuuona kama ishara ya “dharau ya Trump kwa maadili yale yale ambayo maveterani wetu hupigania kuyatetea.”

Jeshi la Wanamaji bado halijatangaza rasmi jina jipya la meli hiyo, na haijajulikana wazi ikiwa meli nyingine za daraja la John Lewis – ambazo zote zimepewa majina ya viongozi wa harakati za haki za kiraia – nazo zitabadilishwa majina.

Meli nyingine katika kundi hilo zimepewa majina ya kiongozi wa haki za Wamarekani Weusi John Lewis, aliyewahi kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Juu Earl Warren, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Marekani na Seneta Robert F. Kennedy, pamoja na wanaharakati wa haki za wanawake na wapinga utumwa Lucy Stone na Sojourner Truth.





Comments