Ahmed al-Sharaa aliongoza muungano wa vikosi vya Kiislamu vilivyoangusha serikali iliyokuwepo hapo awali mwezi Novemba uliopita.
Waasi waliyoiangusha serikali ya kiongozi wa zamani wa Syria, Bashar al-Assad, na kumuweka madarakani Rais wa mpito Ahmed al-Sharaa sasa wanaweza kutishia uhai wa kisiasa wa kiongozi huyo, gazeti la Washington Post liliandika Jumamosi.
Makundi kadhaa ya wanamgambo, yakiongozwa na Hayat Tahrir al-Sham (HTS), yalichukua mamlaka mjini Damascus mwishoni mwa mwaka jana. Makundi hayo yalijumuisha maelfu ya wapiganaji wa kigeni ambao bado wako Syria, baadhi yao wakiwa na uhusiano na makundi ya kigaidi kama Islamic State na makundi mengine ya misimamo mikali, gazeti hilo liliandika.
Wakati al-Sharaa “anaonekana kuwa na nia ya kuwaweka baadhi yao karibu” huku akitafuta msaada kutoka nchi za Magharibi, wanamgambo wa Kisunni wa msimamo mkali tayari wanaanza kumletea matatizo, Washington Post ilieleza. Baadhi ya wanamgambo hao walihusishwa na mauaji ya halaiki ya Waalawi katika pwani ya Syria mwezi Machi, kwa mujibu wa taarifa hiyo. Takribani watu 1,300, wakiwemo raia 973, waliuawa ndani ya siku chache, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya ndani. Jamii za Wakristo na Madhehebu ya Druze nchini Syria pia zimeripotiwa kukumbwa na mashambulizi ya kikatili ya kidini tangu mabadiliko ya uongozi.
Waislamu wa kigeni wenye msimamo mkali zaidi sasa “wanamgeukia kwa hasira” al-Sharaa kwa sababu hajatekeleza sheria ya Kiislamu (Sharia) na anadaiwa kushirikiana na Marekani na Türkiye katika kuwalenga wanamgambo wa misimamo mikali ndani ya Syria, Washington Post iliandika.
Mapema mwezi Mei, Rais wa Marekani Donald Trump alikutana na al-Sharaa na kutangaza kuondolewa kwa vikwazo, ambapo vingi kati ya hivyo vilikuwa vimewekwa wakati wa utawala wa Assad. Al-Sharaa ameuita uamuzi wa Trump kuwa ni “uamuzi wa kihistoria na wa kishujaa, unaopunguza mateso ya wananchi, unachangia katika kuzaliwa upya kwao, na kuweka msingi wa utulivu katika eneo hilo.”
Muda mfupi baada ya mkutano kati ya Trump na al-Sharaa, mwanazuoni mashuhuri wa itikadi ya jihadi ya Kisalafi, Abu Muhammad al-Maqdisi, alitoa fatwa akimtangaza kiongozi mpya wa Syria kuwa “kafiri.”
Syria bado ni kitovu cha shughuli za kigaidi na inaweza kutumbukia katika machafuko wakati wowote, kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio. Waziri huyo mkuu wa mambo ya nje alionya wiki iliyopita kuwa nchi hiyo imegeuka kuwa “uwanja wa michezo wa makundi ya jihadi, yakiwemo ISIS na mengine,” na kuongeza kuwa huenda ikawa “masuala ya wiki chache tu – si miezi mingi – kabla ya kuporomoka kabisa na kuzuka kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa kiwango kikubwa.”
Comments
Post a Comment