Afrika Kusini imeteua majaji maalum kuchunguza madai ya uonevu na ukandamizaji wa haki uliofanyika wakati wa utawala wa ubaguzi wa rangi (apartheid).

Kiongozi wa nchi amesema ucheleweshaji wa mashitaka ya kihistoria umeleta maumivu kwa familia za waathirika. 


Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini amemteua Jaji mstaafu wa Mahakama ya Katiba, Sisi Khampepe, kuongoza uchunguzi maalum kuhusu ucheleweshaji wa uchunguzi na mashitaka ya uhalifu wa enzi ya ubaguzi wa rangi (apartheid).

Khampepe atasaidiwa na Jaji mstaafu Frans Diale Kgomo na Wakili Mkuu Andrea Gabriel SC. Tume hii itachunguza matukio kuanzia mwaka 2003 hadi sasa.

Ramaphosa amesema tume hii ni sehemu ya makubaliano yaliyofikiwa mahakamani na familia za waathirika wa uhalifu wa apartheid, ambazo ziliwasilisha kesi dhidi ya serikali. Amesisitiza kuwa madai ya kuingiliwa kwa mashitaka haya yamechelewesha haki kwa waathirika, na kusababisha maumivu makubwa kwa familia zao.

Majukumu ya tume ni pamoja na kuchunguza:

  • Kama kulikuwa na juhudi za kuzuia uchunguzi na mashitaka ya kesi za TRC;

  • Ni nani waliohusika na kwa nini;

  • Kama maafisa wa polisi au waendesha mashitaka walishirikiana kinyume na sheria;

  • Ikiwa hatua zaidi zinapaswa kuchukuliwa, kama vile mashitaka mapya;

  • Na kama waathirika wanastahili fidia ya kikatiba, na kiasi chake.

Ramaphosa amesema lengo ni kuleta ukweli, haki na mwongozo kwa hatua zaidi zitakazofuata.

Waathirika na familia zao walio na maslahi katika kesi za Tume ya Ukweli na Maridhiano (TRC), wakiwemo wanaoshiriki katika mashauri yanayoendelea mahakamani, ni miongoni mwa wadau wakuu wa uchunguzi huu.

Tume ya Uchunguzi, ambayo imeanzishwa kwa makubaliano kati ya serikali na familia za waathirika, imepewa miezi sita kukamilisha kazi yake na inapaswa kuwasilisha ripoti yake ndani ya siku 60 baada ya kumaliza kazi hiyo.

Ingawa pande zote mbili – serikali na familia za waathirika – walikubaliana juu ya kuanzishwa kwa tume hii, bado kuna masuala ambayo hayajatatuliwa: serikali inaona ni ya kushughulikiwa na tume, ilhali familia zinataka yapelekwe mahakamani.

Tume ilipoanza kazi rasmi, serikali ilikaribisha ahadi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (NPA) na Jeshi la Polisi (SAPS) ya kuendelea kuchunguza na kufuatilia kwa mashitaka kesi za TRC ambazo bado hazijashughulikiwa, huku rasilimali maalum zikiwa tayari zimetengwa kwa ajili ya masuala ya kipaumbele.

Rais Ramaphosa alisisitiza umuhimu wa kuwawajibisha wale waliofanya uhalifu wakati wa apartheid bila msamaha wa kisheria, na akatumaini kuwa uchunguzi huu utasaidia kufichua ukweli na kuleta mwafaka kwa kipindi cha machungu katika historia ya taifa.

Comments